MwanzoContactsEmail
Home Uchambuzi Maoni ya Mhariri Tanesco sasa imekuwa mzigo usiobebeka
BOOKMARK THIS PAGE
Tanesco sasa imekuwa mzigo usiobebeka  Send to a friend
Tuesday, 31 August 2010 21:46

Kwa wiki kadhaa sasa, wadau wa nishati ya umeme katika mikoa kadhaa hapa nchini wamekuwa wakikutana na watendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura), kujadili na kutoa mapendekezo yao kuhusu maombi ya Tanesco ya kupandisha bei ya umeme kwa wastani wa asilimia 34.6 mwaka kesho, asilimia 13.8 mwaka 2012, na asilimia 13.9 mwaka unaofuata.Mikutano hiyo ambayo imefanyika katika mikoa ya Dar es Salaam, Tabora, Mbeya,

Mwanza na Kilimanjaro, licha ya kupokea maoni na mapendekezo ya wadau kuhusu maombi hayo ya Tanesco ya kupandisha bei ya umeme katika muda wa miaka mitatu ijayo, ilikuwa pia na lengo la kutekeleza azma ya Serikali  ya kuimarisha utawala bora nchini kwa kuwashirikisha  wananchi katika maamuzi mazito kama ya kurekebisha bei za huduma ya umeme kwa kutoa maoni yao kwa uwazi na pasipo kificho.

Kwa mujibu wa Ewura, uongozi wa Tanesco umesema kwamba mapendekezo yao hayo yanalenga kuliwezesha shirika hilo kutekeleza kile inachokiita mkakati wake wa kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za umeme nchini, ili miundombinu iliyopo sasa iweze kuboreshwa, pamoja na kuongezwa nyingine mipya ili kupeleka huduma katika maeneo ambako hazijafika.

Maombi kama hayo mara nyingi huletwa pasipo uchambuzi wa kutosha, kwa maana ya sababu hasa za kupandisha bei hizo wakati huo na kwa kiwango hicho. Aghalabu ni zoezi linalofanyika kwa mazoea tu kwa Tanesco kuomba kupandisha gharama za umeme kwa viwango vikubwa mno kwa mkupuo.

Itakumbukwa kwamba mara ya mwisho shirika hilo liliwasilisha maombi Ewura kupandisha bei za huduma ya umeme mwaka 2007 kwa wastani wa asilimia 40 kwa wateja wote. Ewura, pasipo kuangalia kwa undani sababu za ombi hilo na pingamizi zilizowekwa na wadau na vyombo husika,

iliidhinisha  ongezeko la asilimia 21.7 ambalo, kwa tafsiri yoyote ile,  bado lilikuwa ni kubwa mno. Hata baada ya Ewura kuitaka Tanesco kuandaa na kutekeleza kile ilichokiita Mkataba wa Huduma kwa Wateja ili kuwawezesha kupata thamani halisi ya fedha zao, bado shirika hilo liliendelea kusuasua.     

 Ndiyo maana maombi ya hivi sasa ya shirika hilo kwa Ewura yamepingwa vikali na wadau wote katika mikoa yote tuliyoitaja hapo juu. Baraza la Ushauri la Watumiaji wa Huduma Zinazodhibitiwa na Ewura (Ewura-ccc), limepinga maombi ya shirika hilo na kusema kwamba wafanyakazi  wake ndiyo wamesababisha lisifanye kazi kwa ufanisi.

Wadau sasa wanaiona Tanesco kama mtoto wa Ewura asiyetaka kukua na kujitegemea, ambaye anadeka kwa sababu anapewa kila anachokihitaji wakati wowote.  Pingamizi hilo limekuja wakati shirika hilo likihaha kutafuta zaidi ya sh16 trilioni kwa ajili ya kile linachokiita mpango kabambe wa kusambaza umeme nchini.

Pamoja na pingamizi hilo, wadau wanashindwa kuelewa kwa nini shirika hilo linashindwa kubuni na kutafuta mikakati ya kujiongezea mapato na kujiendesha kibiashara. Kwa mfano, wakati mtendaji mkuu wa shirika hilo,

William Mhando, alitangaza hivi karibuni kwamba shirika lake linawadai wateja wake zaidi ya sh300 bilioni, hakusema kwa nini limeshindwa kukusanya deni hilo, mbali ya kufahamu siyo tu majina yao, bali pia sehemu wanazoishi wadeni wake hao.

  Sisi tunasema kwamba shirika hilo sasa ni mzigo mkubwa usioweza kubebwa tena na wananchi. Badala ya kuyakubali maombi ya Tanesco,

Ewura ilishauri shirika hilo kuwaachisha kazi wafanyakazi wake wasio waaminifu ambao, kwa mfano, wanawaunganishia wateja umeme kinyemela. Pia, shirika hilo lishauriwe kupunguza wafanyakazi,

kwani idadi yao ipatao 5,338  ni kubwa mno. Iwapo litaboresha huduma kwa wateja na kuacha visingizio vya uhaba wa mita, nguzo, na nyaya za umeme, litaweza kujikwamua katika matatizo lililomo hivi sasa.

Add this page to your favorite Social Bookmarking websites
Reddit! Del.icio.us! Mixx! Free and Open Source Software News Google! Live! Facebook! StumbleUpon! TwitThis Joomla Free PHP
 

Add comment

Tumia jukwaa ili kutoa maoni ambayo yatasaidia kulijenga taifa letu. Kumbuka, maoni yako yatapitiwa kwanza kabla hayajarushwa hewani!!!!!!


Banner