|
26 kuwakilisha Tanzania Madola |
Send to a friend |
|
Thursday, 02 September 2010 21:41 |
|
Clara Alphonce KAMATI ya Olimpiki Tanzania imetuma majina 26 katika Kamati ya Olimpiki India kwa ajili ya mashindano ya Jumuiya ya Madola itakayofanyika nchini humo Oktoba 3 mwaka huu.
Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania, TOC, Filbert Bayi alisema kuwa walitakiwa kutuma majina 30 lakini wameshindwa kutuma majina wachezaji watatu na kocha mmoja kwa sababu hayakuwepo katika orodha ya awali waliyoituma mapema Mei kwa ajili ya kuthibitisha ushiriki.
Alisema kuwa michezo hiyo inashirikisha mataifa 71 wanachama wa Jumuiya ya Madola na timu inaondoka nchini Septemba 26 kwenda nchini India.
Wachezaji ambao majina yao hayajatumwa ni Frank Martin, Barae Hami (riadha), Haruna Swanga (ngumi) na kocha Ramadhani Othman.
Bayi alisema kuwa majina yaliotumwa kwa upande wa ngumi ni saba, riadha wanane, meza sita, kuogelea wanne wakati timu ya walemavu itakuwa na wachezaji wawili.
Tayari timu zote zipo kambini katika hoteli ya Durban jijini Dar es Salaam, riadha wapo Arusha katika hoteli ya Safari na timu ya meza bado kuingia kambini.
Jumla ya wanariadha 10 wameingia kambini Arusha tayari kwa michezo hiyo na watashiriki katika mbio za marathon, mita 10,000, 5000, 1500 pamoja na mita 800.
Wanariadha hao ni Samson Ramadhan, Shamba Nyange, Michael Joseph, Dikson Marwa, Chepe Dunia, Restituta Joseph, Zakia Mrisho na Frank Martin.
|