|
Ibrahim Yamola SERIKALI imeridhia kurudisha michango kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari jijini Dar es Salaam na kufuta malipo wanayotozwa kwa ajili ya masomo ya ziada.Tamko hilo lilitolewa jana na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Philipo Mulugo alipokuwa akizungumza na wakuu wa shule za msingi na sekondari jijini Dar es Salaam.
"Lakini michango hii yote ihakikishwe inatolewa kwa risiti ili nitakapokuja kutembelea, ama mzazi akitaka kujua matumizi, aonyeshwe kihalali na sio kuchukua fedha hizo na kuzitumia mnavyojua,” alionya naibu waziri huyo.
Alitaja michango inayoruhusiwa na viwango vyake kwenye mabano kuwa ni tahadhari (Sh5,000), taaluma (Sh15,000), vitambulisho (Sh5,000), nembo ya shule (Sh2,000) na madawati (Sh15,000) . Alisema fedha hizo zinapaswa kutolewa kabla wanafunzi hawajaanza masomo.
Alisema pamoja na michango hiyo, bado sehemu kubwa ya fedha hizo itaendelea kutolewa na Serikali. “Jumla ya gharama ya fedha za madawati ni Sh70,000 lakini mwanafunzi anapochangia Sh15,000 kiasi kingine cha Sh55,000 kinatolewa na Serikali hivyo kwa kuwa elimu yetu ni ya kuchangia, ndio maana inatulazimu wazazi kushirikiana katika hili,” alisema Mulugo.
Hata hivyo naibu waziri huyo ameagiza kuwa michango hiyo yote, lazima ipate baraka za kamati na bodi za shule. Alieleza kuwa uamuzi huo wa Serikali umefikiwa baada ya mvutano mkali kati yake, wazazi na walimu. Alifafanua kuwa mvutano huo umetokana na tofauti ya michango hiyo kutoka shule moja hadi nyingine, hivyo Serikali kuamua kuja na uwiano ili kuondoa tofauti hizo.
"Wizara kwa kushirikiana na walimu wakuu, tumekubaliana kuendeela kutolewa michango kwa masharti ya kuhusisha kwanza bodi za shule na wazazi kabla ya kuanza kutolewa,” alisema Mulugo. Alifafanua kwamba zoezi hili la michango kwa shule za msingi na sekondari, litaanzia jijini Dar es Salaam na baadaye kusambaa nchi nzima.
Kuhusu tuisheni Katika mkutano huo, Mulugo aliagiza kukoma mara moja utaratibu wa kuwalazimisha wanafunzi kulipia tuisheni ambazo zimekuwa zikifundishwa katika shule mbalimbali, wakati wa vipindi vya masomo, hususani muda wa asubuhi. “Hizo fedha mnazowatoza watoto kwa ajili ya kulipia tuisheni wakati wa asubuhi, iwe mwanzo na mwisho, labda kwa muda wa jioni, kwani kufanya hivyo ni kukiuka maadili. Atakayebainika kupuuza agizo hii atachukuliwa hatua kali,” alionya Mulugo.
Alitaka pia michango ya Sh200 kwa ajili ya mitihani inayotozwa kwa baadhi ya shule, ikome badala yake wanafunzi wafanye mitihani hiyo bure.
“Mwalimu anayetaka wanafunzi wake kufanya vizuri ni lazima awape mazoezi mengi na moja ya hayo, ni kuwafanyisha mitihani, hivyo hakuna haja ya kuwatoza gharama hizo na kuanzia sasa itakuwa ni bure,” alisema Mulugo. Hatua hiyo ya Mulugo kuwaita wakuu wa shule kujadili kuhusu michango hiyo, imekuja baada ya ziara ya siku mbili jijini Dar es Salaam ambapo alibaini kuwepo michango mingi batili.
Katika hatua nyingine, naibu waziri huyo amepiga marufuku shule yoyote kusajili wanafunzi kabla haijapata usajili na kuzitaka shule zinazopokea wanafunzi kutoka shule zisizosajiliwa, kuacha jambo hilo mara moja.
"Pia ni marufuku (shule zisizokuwa na usajili) kudahili wanafunzi kabla hujasajiliwa na wale waliosajiliwa, marufuku kupokea wanafunzi wanaotoka kwenye shule zisizosajiliwa," alisema.
Katika siku za karibuni wananchi katika maeneo mengi nchini, wamekuwa wakilalamikia viwango vya michango vinavyotozwa katika shule mbalimbali kwa sasa kwamba havieleweki.Baadhi ya wazazi na walezi hao, wamekwenda mbali zaidi na kueleza kuwa , hivi sasa wanalipa pesa nyingi tofauti na kipindi ambacho Serikali ilikuwa haijatangazwa kufutwa kwa ada shule za msingi na kupunguzwa kwa zile za sekondari.
Wananchi hao wamekuwa wakiitaka Serikali kubainisha viwango maalumu vinavyopaswa kuchangiwa kwenye shule hizo ili kuondoa mkanganyiko wa michango mingi isiyoeleweka.
|