|
Watalii waongezeka mlima Kilimanjaro |
Send to a friend |
|
Saturday, 28 January 2012 08:55 |
|
Rehema Matowo, Marangu WATALII 33,326 wamepanda mlima Kilimanjaro kuanzia Julai mwaka jana hadi Desemba 2011, ikiwa ni ongezeko la asilimia 29.8.
Katika taarifa yake kwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, Mhifadhi Mkuu wa Kinapa, Nyamakumbati Maphuru, alisema kati ya idadi hiyo, 31,423 ni kutoka nje ya nchi na 1,903 ni Watanzania.
Maphuru alisema wamefanikiwa kuingiza zaidi ya Sh30.5 bilioni kwa kipindi cha miezi sita na kwamba, mapato yamekuwa yakiongezeka kila mwaka, kipindi cha mwaka 2000 pato liliongezeka kutoka Sh7.1 bilioni hadi Sh45.6 bilioni, ikiwa ni ongezeko la asilimia 538.3 kwa kipindi cha miaka kumi.
Kuhusu hali ya uokoaji ndani ya mlima, Maphuru alisema watalii 1,776 kutoka ndani na nje ya nchi waliokolewa kutokana na matatizo mbalimbali ya afya hasa kwa magonjwa yaliyosababishwa na upungufu wa hewa ya oksijeni. Aliongeza kuwa miongoni mwa waliookolewa, watatu walipoteza maisha akiwamo Mtanzania mmoja ambaye ni mpagazi baada ya mapafu yake kujaa maji, huku raia kutoka Uingereza walikufa kwa kupata mshutuko wa moyo na mwingine mapafu kujaa maji na kushindwa kupumua.
Maphuru alisema hifadhi inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwamo kuwapo kwa matukio ya ujangili hasa ukataji miti ya asili na uchomaji moto msitu.
Changamoto nyingine, ni wananchi kuchunga mifugo hifadhini kinyume cha sheria na uduni wa baadhi ya miundombinu ya kuhudumia watalii hasa kwenye lango la Mweka, Londorosi na Kitiuo cha Rongai.
|